Friday, December 27, 2013

FASIHI YA KISWAHILI


 FASIHI YA KISWAHILI

SWALI:  Je, kuna umviringo wowote katika fasihi ya mwafrika? Kama upo ni katika maeneo yapi? Rejea ujumi katika fasihi mifano yako ijikite Katika mila na desturi za wasafwa na Wanyakyusa.                                                                                       

DONDOO

          UTANGULIZI
Ø      Historia fupi ya Wanyakyusa na Wasafwa.
Ø      Dhana ya umviringo katika Fasihi simulizi.

  KIINI
Ø      Maeneo yanayothibitisha uwepo wa umviringo katika fasihi simulizi ya Wasafwa na Wanyakyusa.


        HITIMISHO
       
        MAREJEO                                                                                                                                                                                            










Wanyakyusa ni kabila linalopatikana nyanda za juu kusini magharibi mwa Tanzania tangu karne ya 10. Walitokea nchini Malawi kusini mwa ziwa Nyasa wakijulikana kama Wangonde. Kutokana na wenyeji waliowakuta (Wasafwa na Wanyamwanga) kuwaita Wanyasa jina la kabila lao lilibadilka. Waliamua kuboresha jina la kabila lao (Wanyasa) kwa kuchopeka herufi za kiongozi wao wa kidini (Kyungu) na kuwa Wanyakyusa (waumini kutoka Nyasa). Kuja kwao katika maeneo ya kabila la Wasafwa naWanyamwanga kulisababisha kutoelewana nao kwa sababu ya majigambo yao. Hata hivyo, tofauti zao zilimalizika kwa sababu ya kuungana dhidi ya biashara ya utumwa na Wangoni ambao waliwavamia wakazi wa mkoa wa Mbeya. Mpaka sasa Wanyakyusa wamechangamana sana na Wasafwa, Wanyamwanga na makabila mbalimbali ya Tanzania kutokana na shughuli za kiuchumi, kijamii na kiutawala.  (www.habarileo.co.tz/index.php.makala/14765-wanyakyusa)

Aidha, Wasafwa ni wenyeji hasa wa mkoa wa Mbeya mjini na makabila mengine ni wahamiaji tu kutoka sehemu mbalimbali. Aidha, kutokana na Wahehe kupigwa sana na Wasangu wakisaidiwa na Wajerumani ambao walipigwa kibabe na katika maeneo ya Lugalo Iringa, ilisababisha Wasafwa wengi kukimbilia maeneo ya milimani. Jambo hili lilisababisha Wasafwa kuwa washamba na wachafu pia. Wasafwa wamegawanyika katika makundi mbalimbali kutegemea na sehemu wanazoishi na ndiyo maana kuna wasafwa wa Ilomba, Mbalizi na maeneo mengine. Kuongea kwao hutofautiana, wengine huongea kwa kuvuta lakini wengine kuharakisha lakini wanaelewana wote ni wamoja.  

Mviringo ni dhana inayoturudisha palepale, dhana hii tunaiona katika saa, siku, miezi, miaka na karne (Kezilahabi, 2002:165). Hivyo, umvirngo katika fasihi simulizi ya Mwafrika ni hali ya kujirudiarudia kwa tendo au namna ya nyanja za maisha, kiutamaduni, kisiasa na kijamii. Umviringo huu huenda sanjari na ujumi katika kazi za fasihi simulizi.

Katika eneo la utawala au uongozi umviringo unajidhihirisha katika upatikanaji wa viongozi kwa njia ya kurithishwa. Kurithishwa huku hutokea ndani ya ukoo wa mtawala. Kwa mfano utawala katika jamii ya Wasafwa ulikuwa kwa muundo wa kichifu. Familia za kichifu ziliogopwwa sana kiuchawi, na Wasafwa zamani walikuwa na imani ya uchawi sana. Pia, kulikuwa na waganga wa miti shamba wa uhakika. Zamani hizo ambapo chifu Mwanshinga mhamiaji kutoka Ukinga alipofika maeneo ya Wasafwa yeye ndiye aliyewasha moto kwa mara ya kwanza Usafwani. Pia alikuja na mbegu katika nywele zake ambazo hakuwahi kuzikata tangu azaliwe. Kutokana na maajabu hayo akatoroshwa na baba yake na kuhamia Usafwani na ndicho chanzo cha ukoo wa Mwanshinga.
          “Umwene umwinza wuwula wakupapwa ishimwene”

            “Chifu mzuri ni yule anayezaliwa kichifu”

Kwa hiyo, katika kuendeleza uongozi kwa Wasafwa ilibidi mrithi wa chifu atoke ndani ya familia ya kichifu na awe amezaliwa kichifu, mfano azaliwe akiwa ameota meno.


Vilevile simulizi za Wanyakyusa zinasisitiza utawala wa mfumo dume. Mwanaume ndiye kichwa cha familia na ndiye mwenye maamuzi katika familia.
     “Wanyakyusa wameshawahi kuwa na kiongozi mwanamke anayefaahamika
       kwa jina la Nyanseba. Inasemekana kuwa kiongozi huyo alijaribu kuweka
       utawala wa mfumo jike, lakini hakufanikiwa kwa kuwa alipinduliwa na
       wasaidizi wake ambao waliweka dola la mfumo wa utawala wa kifalme” (habarileo.co.tz)
Kwa maana hiyo umviringo katika uongozi kwa pande za makabila yote mawili unajidhihirisha kwa kitendo cha kurithishana majukumu kutoka kizazi kimoja kwenda kingine.

Dhana ya wakati katika fasihi simulizi inaonesha umviringo na ujumi katika fasihi. Tunaiona katika saa, siku na karne. Mfano katika kabila la Wanyakyusa suala la wakati linatumika katika uvunaji wa mazao (mfunjo) kwa kila mwaka. Kwa mfano mwezi wa pili, tatu na nne ni kipindi cha mavuno ya mahindi ambacho kila mwaka kinajirudia. Kuanzia mwezi wa saba na wa nane ni kipindi cha mavuno ya maharage ambapo kipindi hiki hujirudia kwa kila mwaka. Hivyo dhana ya wakati ilikuwa inatumika kwa mtindo huo na inajidhihirisha kuwa ni mviringo kwa kuwa kila mwaka vipindi hivi hujirudiarudia.

Aidha, kumteua mchumba ni eneo mojawapo linaloonekana kuwepo kwa umviringo. Tamaduni za Kiafrika zinasisitiza kuoa au kuolewa na mtu wa kabila au dini moja. Kwa hiyo basi utamaduni huu upo hata kwa makabila ya Wanykyusa na Wasafwa kwani vijana husisitizwa kuoa au kuolewa miongoni mwa makabila yao wenyewe. Pia, hata wachumba huweza kuchaguliwa na wazazi wao lakini huteuliwa miongoni mwa makabila yao yaani Wanyakyusa au Wasafwa. Malengo ya kufanya hivi ni kulinda utamaduni na kuzuia magonjwa ya kurithishwa.
        “Tamaduni tofauti zimeangalia namana ya kutafuta wachumba au kuoa au
          kuolewa. Baadhi ya jamii uchaguzi wa wachumba hufanywa na wazazi hii
          inaweza kufanyika hata kabla ya kuzaliwa kwa mtoto” (Mbiti, 1971:135).

Pia, majina katika kabila la Wanyakyusa na Wasafwa huwa na desturi ya kurithishwa kutoka mtu mmoja hadi mwingine. Imani yao ni kwamba mtu wa makamo jina lake hupewa mtoto mchanga azaliwaye kwa madhumuni ya kwamba tabia alizonazo mtu huyo wa makamo ambazo kwa mategemeo ya wengi ni zile nzuri hurithiwa na mtoto mchanga aliyezaliwa. Kwa mfano kama jina la ukoo ni Mwakalindile mtumiaji wa jina hilo hurithishwa kwa wajukuu wa kiume ambapo atabakia kuitwa Mwakalindile wakati mtoto wa kike atachukua au atarithi jina la bibi yake. 

Kifo na mazishi ni matukio ambayo yalikuwepo tangu zamani. Kiutamaduni wasafwa walimwogesha marehemu na kumkalisha kwenye kiti kabla ya kucheza ngoma ya msibani. Iwapo mtoto wa kwanza katika familia amefariki maiti huzikwa kwa babu mzaa mama, mtotowa pili akifariki huzikwa kwa babu mzaa baba, mtoto watatu na kuendelea ndio mali ya wazazi husika hivyo ilikuwa ni lazima kuzaa watoto zaidi ya watatu ilifamilia changa ipate mtoto wao.
                                               
           Mfano wa kaburi la Wasafwa likiwa katika umbo la duara ndani ya kaburi la pembe nne.

Sambamba na mzishi haya kufuata mila na desturi za maumbo ya makaburi, kabila la Wasafya hutumia kakavu (tarumbeta) kutoa taarifa kwa wanajamii ili waweze kujua kuwa kuna msiba kijijini.
                        
                 Mfano wa picha ya kakavu (tarumbeta) itumikayo kutoa taarifa ya msiba ikiwa

                 begani kwa mtu wa pili kutoka kulia.

Tukio hili lilijulisha jamii nzima kuhudhuria msiba nyumbani kwa marehemu ambapo marehemu alizikwa nyuma ya nyumba.
                                              
                                Mfano wa picha ya mazishi yanayofanyika nyuma ya nyumba  

Pia, Wanyakyusa wanadesturi ya kumwogesha marehemu kabla ya kumzika. Uwepo wa vipengele vinavyofanana hadi leo kunadokeza umviringo katika Fasihi simulisi zao.

Kwa upande wa kuzika Wanyakyusa walifanya ibada za kimila zikiambatana na matumizi ya unyuso nguo za kufunika maiti. Jambo hili linafanyika hadi leo na nguo hizo ni maarufu kwa jina la sanda.     
       “Marehemu walifungwa nguo iliyotengenezwa kwa magome ya miti
         Inayojulikana kwa jina la unyuso. Nguo hiyo ilitumika kumfunika
         marehemu mithili ya sanda kisha aliwekwa kwenye shimo la duara
         maarufu kwa jina la itago” (www.habarileo.co.tz/index.php/makala/14765-wanyakyusa).
Maumbo ya mashimo ya kuzikia kwa Wanyakyusa yanadokeza umviringo katika fasihi simulizi japo siku hizi taratibu hizi zinadorora siku hadi siku.

Kipengele cha imani na dini nacho kinagusia umviringo katika Fasihi simulizi ya Wanyakyusa na Wasafwa. Kwa asili watu hawa walikuwa na dini na imani zao za asili walisali katika miti mikubwa, mito na makaburini kama njia ya kutatua matatizo yaliyowasonga. Kuingia kwa wamisionari wa kwanza mnamo mwaka 1892 wakiongozwa na Merensky na Nauhans wakiwa na madhehebu ya misheni ya Berlin kulianza kuwabadilisha imani zao hata kabla ya kuja wamisionari wa Morovian (www.habarileo.co.tz/index.php/makala/14765-wanyakyusa).

Hata hivyo, wabantu hawa wanapokubwa na matatizo makubwa kama magonjwa, vifo na magonjwa mengine ambayo hushindikana kutatuliwa kanisani huamua kwenda kwa waganga wa jadi (Tembels, 1959:13). Pia Wasafwa na Wanyakyusa wa sasa bado wanaamini waganga wa jadi licha ya kuokoka. Hili linajidhihilisha wazi kwa jinsi kipindi cha Dr.Mlingolingo kinavyopata wapenzi wengi katika radio Generation FM. Mlingolingo hupokea simu za watu wengi hasa waishio mkoa wa Mbeya licha ya kuwepo kwa makanisa mengi. Dodoso za mganga huyu kwa njia ya simu hudokeza jinsi watu hawa walivyoshindikana katika maombi kanisani huamua kutaka msaada kutoka kwake. Aidha maeneo waliko na majina yao yanadokeza kuwa wapenzi wa kipindi hiki ni Wanyakyusa na Wasafwa hata waliobatizwa na kuokoka.

Vilevile kipengele cha ngoma za Wanyakyusa na Wasafwa kinaonesha ujumi wa duara. Jambo hili linadhihirishwa na jinsi ngoma zao zilivyo na zinavyochezwa. Wanyakyusa wanacheza ngoma za asili ambazo hujulikana Kama Ipenenga na Miparano. Mara nyingi Ipenenga huchezwa na wazee au machifu wa ukoo na huvalia vizuri na kucheza kwa umakini. Miparano huchezwa katika kufurahia mavuno yao. Jambo la msingi hapa ni mkao wao na vifaa wanavyotumia wakati wa mchezo ambavyo hutengenezewa dhana ya mduara. Wachezaji hushika mkongojo na kucheza kwaduara (www.habarileo.co.tz/index.php/makala/14765-wanyakyusa).

Kwa upande wa Wasafwa kuna ngoma zao zinazoitwa Mbeta, Ndingala, Mwadede na Bidubidu. Ngoma hizi mara nyingi zilichezwa wakati wa mavuno na mara chache wakati wa msiba (mwengulo) wa watu maarufu. Hata hivyo, zimepungua kasi kutokana na mwingiliano wa tamaduni na dhana kuwa kuchezwa kwake katika mwengulo kunazidisha haja ya kulogana ili watu wapate kula na kunywa. Jinsi wanavyocheza na vifaa wanavyotumia hudhihirisha mduara katika ngoma. Mwashinga (2012) anasema:
        “mguuni kunavaliwa njuga za chuma za duara (INSAHALA) ambazo
         zinagonganishwa kwa kufuata mlio wa pembe zinazokuwa zinapigwa
          na wanaume na kuleta mziki mzuri. Pembe hizo ndiyo jina lenyewe
          la ngoma yaani MBETA.”  

Mila ya utani imeenea sana kwa Waafrika. Watu wanavyokutana hutanina kwa maneno na vitendo huku wakizingatia masharti yanayotawala uhusiano wa utani huo. Waafrika hutaniana baina ya mtu mmoja na mwingine au kabila moja na kabila jingine. Kwa mfano Wanyakyusa wanataniana baina ya babu na mjukuu wake, bibi na mjukuu wake, pia mashemeji. Aidha, Wanyakyusa huweza kutaniana na Wahehe huku masharti ya uhusiano wa utani yakizingatiwa. Utani huu hujirudiarudia kwa kurithishwa katika jamii zao. Hivyo kufanya ujumi wa mviringo katika fasihi simulizi ya Kiafrika.

Desturi ya kula chakula kwa waafrika inatetea ujumi katika mviringo. Waafrika huwa na mila na desturi za kula chakula kwa kuzunguka mahali palipo na chombo cha chakula. Mfano kabila la Wanyakyusa ambao hula chakula chao maarufu msibani (kande) kwa kuweka katika sinia na watu wanalizunguka wakila kwa kutumia majani ya mgomba ambayo huitwa ndundu. Pia, hunawa maji katika chombo kimoja, baba huanza na watoto wa kiume hufuata. Baadaye mama hufuatiwa na watoto wa kike. Watu hula chakula kwa kutumia chombo kiitwacho lwangabya (sinia). Tendo lile la kunawa hujirudia tena kuanzia baba, mtoto wa kiume, mama na baadaye watoto wa kike. Hivyo basi kujirudia kwa tendo hilo la kunawa kabla ya kula chakula na namna ya ukaaji wakati wa kula kunadhihirisha umviringo wa fasihi simulizi ya Mwaafrika.

Aidha, Wasafwa katika desturi ya kula hutumia baadhi ya vyombo kama vile chungu kikubwa (usuyi). Chungu hiki hutumika kutekea na kutunzia maji na kuwekea pombe pia. Ungo (uveto) uliotengenezwa kwa majani na kamba za porini zinazoufanya uwe imara zaidi. Vifaa hivi hutumika kulia chakula na umbo lake huwa la mviringo na kusadifu ujumi wa mviringo katika fasihi ya Kiafrika.

Maumbo ya vitu katika fasihi ya kiafrika yanadhihirisha uwepo wa umviringo. Kutokana na umbo hilo la mviringo jamii za kiafrika ziliamini kuwa umbo hilo ni zuri. Kwa kuangalia jamii za Kinyakyusa na Kisafwa kuna vitu vyao vingi ambavyo vina umbo la mviringo. Kwa upande wa jamii ya Wanyakyusa kuna vifaa vyao vingi vya umbo la duara kama:
Kiswahili                         Kinyakyusa                                    Matumizi
       Ungo                                uluseko                                             kupepetea
       Chungu                            Syala/videko                                     kutunzia nafaka na kupikia
       Kigoda                             ikikota                                              kukalia
       Kibuyu                             ulupale                                             kutunzia maziwa
       Jiwe la kusagia                 ukwala                                             kusagia nafaka nafaka
       Kata                                 ingata                                              kujitwishia mzigo na kukalishia
                                                                                                        vyungu vya nafaka


                                           
                        Mfano wa picha ya kigoda katika kabila la Wanyakyusa (ikikota) 

                                                              
                                    Mfano wa picha ya chungu (ndeko) kwa kabila la Wanyakyusa    

Aidha vitu vyenye umbo la mviringo hupatikana pia katika jamii ya Wasafwa ambapo baadhi ya vifaa hivyo ni kama ifuatavyo:
Kiswahili                   Kisafwa                       matumizi                                                     
      Chungu                    usayi                              kutunzia na kutekea maji na kuwekea pombe
      Ungo                        uveto                             kupepetea                                                             
      Kikapu                     ishitundu                       kuwekea vitu mbalimbali                                         
      Kikombe                  upandi                           kunywa maji au pombe

Hata nyumba za kale za Wanyakyusa zilikuwa za mduara ambapo chifu alijengewa (isyenge) na nyumba za wake zilijegwa pembeni kuzunguka nyumba ya chifu. Pia kwa upande wa Wasafwa nao walikuwa na nyumba zao ambazo ziliitwa isonze ambazo pia zilijegwa kwa umbo la duara.
                                                               
Mfano wa picha ya    msonge (insyenge) kwa Wanyakyusa, (insonze) kwa Wasafwa

Vitu vyote hapo juu kwa makabila yote vina umbo la umviringo na viliandaliwa kwa umbo hilo kwa kuwa ndilo umbo lililoaminiwa na waafrika kuwa ni zuri.

Aidha umviringo katika kazi za fasihi za Kiafrika inaonekana pia katika nyimbo mbalimbali ambazo zinaweza kuimbwa msibani au kwenye sherehe mfano harusi na ngoma. Katika kutekeleza utanzu huu wa fasihi umviringo hujidhihilisha kwa kuwa nyimbo hizo hurithishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine. Mfano katika kabila la Wanyakyusa mara nyingi sehemu za sherehe huimbwa wimbo ufuatao:
       “lelelele amba
        Ujo tubhapele umwana
         Amba lelelele…amba
         Mungu nkomagha
         Amba lelelele…amba
         Mungu mfyundagha
         Amba lelele…amba

Tafsiri yake.
           Mtoto huyo tumewapa
           Ambaa…lelele
            Msimpige
           Ambaa…lelele
           Msimfinye
           Ambaa.lelele

Umviringo pia hujidhihirisha kwa upande wa nyimbo za Wasafwa. Mavazi yao huonekana hadi wakati huu kutokana na baadhi ya Wasafwa kuendeleza tamaduni hizo kwa mfano; kuvaa kitambaa kilichorembwa shanga (Igoyi), mguuni kuvaliwa njuga za chuma za duara (Insahala), kupuliza pembe (Mbeta).

Kuna vifaa mbalimbali vinavyotumika katika kufanya matambiko kwa kabila la Wanyakyusa ambapo hufanyika kama kuna tatizo limetokea kama vile njaa, ukame na magonjwa. Mfano wa vifaa hivyo ni pamoja na vibuyu (kata), moto, ndizi na pombe. Jamii ya Wanyakyusa ilitumia moto kama kifaa cha tambiko katika kuomba Mungu wao. Moto huu ulikokwa na chifu wakati wa kutambika na mara baada ya majibu mazuri ya maombi yao, walichukua moto huo na kurudi nao kijijini. Huko uliandaliwa moto mwingine nyumbani kwa chifu ambao ulitumiwa na wanakijiji wote kuwasha moto huo kama ishara ya kufurahia kutii maombi waliyojibiwa na miungu wao. Umviringo unaozungumziwa hapa ni moto unapozungushwa toka nyumba moja hadi nyingine.

Sambamba na hilo matumizi ya vibuyu (kata) vilivyotumika kunywea pombe wakati wa tambiko vilikuwa na umbo la duara na hata wakati wa kunywa pombe hizo walikaa mkao wa duara. Kwa upande wa Wasafwa ibada za matambiko zilifanyika kuendana na tukio lililoikumba jamii hiyo. Mfano wa matukio hayo ni njaa, ukame na magonjwa katika jamii. Kuhusu suala la ukame chifu (mwene) wa Wasafwa aliwaita wafuasi wake kujadili namna ya kulitatua tatizo hilo, wakati mwingine kulikuwako na watu waliosadika kwamba walitumiwa na mizimu kuleta taarifa juu ya jamii fulani.
       “mzimu (izimu) ni watu ambao walikufa ambao inasadikika kwamba
          nafsi zao zinarudi kwa kupitia mwili au ufahamu wa mtu mwingine
          na kutoa ujumbe kwa ndugu zao ambao wako hai bado” (Mwasinga, 2011:20)

Katika suala hili umviringo unajidhihirisha pale ambapo nafsi ya mtu aliyekufa kurudi kwa aliye hai.

Usimuliaji wa hadidhi upo katika hali ya umviringo hasa katika maeneo mbalimbali. Hadidhi hurithiwa kutoka kizazi kimoja kwenda kizazi kingine, hasa kutoka kwa watu wakubwa kwenda kwa watoto. Pia eneo la hadithi na mtindo wa ukaaji ni wa mviringo kwani hadithi husimuliwa wakati wa jioni wakiwa wameuzunguka moto kwa umbo la duara jambo hili hufanyika ili kumsaidia kila mtoto kushiriki katika usimulizi wa hadithi hizo. Mfano hadithi ya Kinyakyusa huadithiwa kama ifuatavyo:
“Kapango kapango:
Ijolo alipo bhabha jumo alinumwana unyambala bho akulile kafikile  akabhlilo ka kwegha, bhabha ghwake alimbulile ukuti atikulondighwa ukwegha kutali,(ikikolokyapanja)ghwegheghe unyakyusa,lelo umwene akanile ukwegha unyakyusa abhukile ikikolo kyapanja, bhoafikile munjila alimwaghile undindwana jumo bhalina mama ghwake pasi pa mpiki pakaja pa myabho.Alinganile nukulonda ukumwegha,bho alalusisye ifyuma, mama jula atile ungasosya ufyuma nafimo loli kumpimba mpaka kumyenu. Loli bhobhafikile munjila undindwana jula akanile ukusuluka alyandile ukwimba”
             “ Ghwali nyeghile kumyitu x2
              ikisu kya kutukuju kumyetu kula kula x2”
Pitasi unyambala jula alambalele nu ndindwana jula pa nyuma ngimba akalimundu lyali setano. Lyali ngoghile nukwega ubhula bhwake, undumyana jula alinkwenda nu kufwa.

Tafsiri yake kwa lugha ya Kiswahili;
Hadith hadithi:
Hapo zamani za kale palikuwepo na baba mmoja aliyekuwa na mtoto wa kiume. Alipofikia umri wa kuoa baba yake alimwonya kuwa sheria ya Kinyakyusa hairuhusu kuoa nje ya kabila lao lakini yeye alikataa akaondoka kwenda nje ya kabila lake. Alipofika njiani alimkuta binti mmoja na mama yake wakiwa chini ya mti nyumbani kwao. Akampenda yule binti na kuridhia kumuoa. Alipouliza kuhusu mahali yule mama akasema asitoe kitu chochote ila kumbeba hadi nyumbani kwake. Lakini walipofika nyumbani yule binti alikataa kushuka na kuanza kuimba.
      “ulinitoa kwetu x2
        Kaniweke kwangu mji wa Tukuyu, kule kwetu kule x2
Kijana yule baadaye aliamua kulala huku binti akiwa mgongoni. Kumbe hakuwa binti bali ni jini likamuua kwa kumtoa utumbo na ikawa mwisho wa maisha ya yule kijana.

Pia michezo ya watoto hudhihirisha ujumi katika umviringo wa fasihi simulizi ya Mwafrika. Watoto hucheza michezo mbalimbali kifamilia au kwa kukutana na makundi ya familia nyingine. Mfano mzuri ni mchezo ujulikanao kama Azyungule katika kabila la Wasafa, wachezaji hucheza kwa duara. Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana kwa mahojiano tuliyoyafanya na mzee wa Kisafwa Ndele Mengo anayepatikana katika kijiji cha Nzenga kitongoji cha Mbogo, mara nyingi michezo hii hufanyika usiku. Watoto hukusanyika kabla ya chakula cha usiku na kuimba nyimbo mbalimbali huku wakizungukazunguka. Mambo haya yamekuwa yakifanyika tangu zamani hadi sasa. Kwa hiyo umviringo katika fasihi simulizi ya kisafwa inajidhihirisha katika mduara unaotokeza katika michezo yao.
                                            

Kwa upande wa wanyakyusa kuna michezo mbalimbali ya watoto. Watoto hucheza michezo hiyo hasa wanapokuwa hawanashughuli za kufanya.baadhi ya michezo hiyo ni “salo” (mdako) na “kubhasabhasa” au “kudumbadumba”. Namna na vifaa wanavyochezea hudokeza umviringo kwani mashimo ya kuchezea huwa ya duara. Pia, michezo hii bado infanyika hadi leo. Mahojiano yaliyofanyika wakati wa kukusanya data yalidokeza kuwa watoto hucheza mdako kwa kushindana ili kujua ni nani anayeweza kupangua kete huku akidaka nyingine.

Aidha, michezo hii inakuza fikra za watoto na uwezo wa kutenda mambo mengi kwa wakati mmoja.Michezo hii bado ipo hadi sasa hasa kijijini japo kuna michezo mingine inapungua umaarufu kutokana na maingiliano ya tamaduni na utandawazi.

Kwa upande wa Wasafwa elimu ya jando na unyago ilitolewa kwa watoto wa kiume na wa kike. Binti wa Kisafwa baada ya kuvunja ungo aliwekewa ndani peke yake. Ilikuwa ishara inayoonesha kuwa binti akiwa katika siku zake haruhusiwi kupika wala kushiriki na mwenzake katika kazi yoyote ile. Mafunzo yaliyotolewa unyagoni ni pamoja na kufanya kazi kwa bidii, mfano kuchota maji, kutafuta kuni porini na kulima. Ila tohara kwa Wasafwa haikuwepo. Hivyo suala hili la jando na unyago linaendelea katika baadhi yakoo na familia chache ambazo ndizo zinazoendelea na suala hili. Pia kwa upande wa kijana wa Kisafwa mara tu baada ya kubalehe naye huanza kupewa mafunzo ya jando. Akiwa mafunzoni alifundishwa namna ya kujitengemea kama vile kujijengea kinyumba chache (invanza), kuanza kwenda kwenye magita na huko ndiko anaweza akapata mchumba. Suala la tohara kwa kijana wa Kisafwa halikuwepo, lakini baada ya kuanza kujichanganya na makabila mbalimbali limeenea sana kwa watu wote. Hivyo basi kuwepo kwa jando na unyago kunadhihirisha kabisa uwepo wa umviringo wa fasihi simulizi ya Mwafrika.   

Suala la matumizi ya lugha katika fasihi za kiafrika ndani yake kuna umviringo ingawa kutokana na maendeleo ya Sayansi na teknolojia jamii hulazimika kubuni misamiati mipya ili kukidhi mahitaji yao na kuendeleza mawasiliano. Hata hivyo kuna baadhi ya vipengele vya lugha bado vinaendelea kuwa hai hadi sasa, mfano wa vipengele hivyo kwa upande wa wanyakyusa ni;
Vitendawili, mfano i . Inguku jangu jitelile mmifwa (ikinanasi)
                                    Tafsili yake : kuku wangu katagia mibani    (nanasi)
                     Mfano ii. Kunokununu pakati pakali na kuno kununu (isuba)
                                    Tafsili yake : huku kutamu katikati pachungu na mwisho patamu (jua)

Nahau ni kauli zilizojengwa kwa kutumia maneno ya kawaida lakini zinatoa maana isiyo ya kawaida. Mfano i. kinyakyusa:    ali mumbabhu
                              Kiswahili:       yuko kwenye kuni                                                                                                                                                                                  
Maana yake   yuko kwenye siku zake/ yuko mwezini                                                             
              Mfano ii. Kinyakyusa:  Ali na masusu pammilo
                              Kiwsahili:      Ana mavi ya kuku kooni
Maana yake ni binti mdogo asiyeelewa kitu.

Methali nazo huonesha wazi umviringo kwa kurithisha kutoka kizazi kimoja hadi kingine, mfano wa methali ni;
              i. Kinyakyusa: Imbwele ndukama
                 Kiswahili    : Inzi kwenye maziwa
                 Maana yake: Mtu kuingilia jambo lisilomuhusu
              ii.kinyakyusa : Ingongobe jangu nduluka jikukolela bho bhukali
                 Kiswahili    : Jogoo wangu anawika kabla ya wakati
Maana yake ni kusherehekea kabla ya mafanikio.

Aidha kwa upande wa Wasafwa kumekuwa na umviringo katika matumizi ya lugha kwa kuendelea kutumia baadhi ya vipengele japokuwa kuna mabadiliko na maboresho kwa baadhi ya vipengele vya lugha. Mfano wa vipengele vya lugha ambavyo vina umviringo ni; vitendawili, nahau, misemo na methali. Mfano wa misemo Kisafwa: hwasha hwalenga (kumekucha)
                                               Nkulembela zitonela enyau (ukizubaa wajanja watachukua nafasi)
Kwa kuchunguza vipengele vyote vya lugha vilivyofafanuliwa hapo juu ni wazi kuwa umviringo unapatikana kwani kizazi kipya hupata tanzu hizo kwa kurithishwa kizazi kimoja hadi kizazi kingine.
 
Umviringo katika fasihi za kiafrika hujionesha pia katika maleba/mavazi yanayotumika katika utambaji wa baadhi ya tanzu za fasihi simulizi. Ukweli wa jambo hili unajibainisha kwa kutumia kabila la Wanyakyusa na Wasafwa. Kwa upande wa Wanyakyusa kwa kawaida katika uchezaji wa ngoma kuna vifaa kama vile; njuga, mkia wa fisi, mkwiju, filimbi, kaptura na shati jeupe, ngoma za asili.

Aidha kwa upande wa kabila la kisafwa kuna matumizi ya maleba pia ambayo nao huyatumia katika uchezaji wa ngoma. Mfano wa malena hayo ni: njuga, malimba, filimbi na ngoma. Hivyo katika eneo hili umviringo unajitokeza kwa kuwa vifaa hivyo bado vinatumika hadi sasa ingawa kumekuwa na maboresho kidogo kutokana na maendeleo ya sayansi na teknolojia, kwa mfano badala ya kutumia ngoma za asili kwa sasa huweza kutengeneza muziki kwa kutumia kinakilishi na nyimbo nazo hurekodiwa kwenye vinasa sauti na kanda.

Kupambana na mfumo dume nako hudokeza umviringo katika fasihi simulizi za Wasafwa na Wanyakyusa. Kihistoria, Wanyakyusa wamekuwa wakipambana na mfumo dume tangu zamani hasa kupitia kipengele cha majina. Watoto wa kiume hurithi majina ya upande wa ma mfumo mama ilihali watoto wa kike hurithi majina ya upande wa baba zao. Simulizi zinamtaja mwanamke ( Nyaseba) aliyewahi kujaribu kuweka mfumo jike, suala hili bado linajitokeza hadi leo japo limekuwa changamani. Siku hizi wanawake wa Kinyakyusa na Kisafwa wanapambana na mfumo dume kupitia asasi mbalimbali zinazotetea wanawake nchini na ulimwenguni kwa ujumla. Uchunguzi uliofanywa na gazeti la Habarileo gwiji la habari linataja juhudi hizi:
                    ……… wanawake wa kinyakyusa wanaungana na wanawake
                    ulimwenguni kote kukabiliana na changamoto ykubwa ya mfumo
                    dume na kujenga mfumo unaozingatia haki na usawa hasa katika
                    upatikanaji wa elimu, haki ya kumiliki ardhi, mali na kushika
                    nafasi za kutoa maamuzi.(www.habarileo.co.tz/index.php/makala/14765-wanyakyusa)


Kwa kuhitimisha, suala la umviringo katika fasihi simulizi ya kiafrika huweza kujitokeza katika makabila mbalimbali ya Tanzania na Afrika kwa ujumla. Hivyo basi si makabila ya Wasafwa na Wanyakyusa tu ambapo umviringo huweza kujitokeza katika maeneo mbalimbali. Haa hivyo, kutokana na kuingia kwa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia suala hili la umviringo limeanza kupungua siku hadi siku.    


 

















MAREJEO
Kezilahabi , E.(2002), Makala ya Nadharia ya Fasihi Simulizi na Maendeleo katika Sayansi na
                                     Teknolojia, TUKI, Dar es salaam.

Mbiti, J. S. (1971), African Religions and philosophy, Heinemann Educational Book Ltd, Nairobi.

Msokile, M. (1992), Misingi ya Hadithi Fupi, Dar es Salaam University Press, Dar es Salaam.

Mwanshinga, S. P. (2012), Wajue Wasafwa Kutoka Mbeya.

Ngure, A. (2006), Fasihi Simulizi Kwa Shule Za Sekondari, Phoenex publishers Ltd, Nairobi.

Tembles, P. (1954), BantuPhilosophy, Presence Afrcaine Kutoka
                        www.aequtoria.be/temples/BiblioDetemplesEnglish.html. 16.10.2013 saa 15:00

                                                     

www.safarilands.org/docs/jamii-ya -wasangu-tanzania.pdf.20/10/2013 saa16:30.

1 comment:

.... said...

Nilichanganyikiwa na kuhuzunika mume wangu alipoomba talaka. Kisha nikawasiliana na Dk DAWN, baada ya kuona ushuhuda mwingi wa jinsi Dk DAWN alivyosaidia watu wengi kurejesha amani katika ndoa na uhusiano wao,
Pia niliona jinsi alivyotibu magonjwa mbalimbali na kusaidia watu wachache kutibu ugumba, niliamua kuwasiliana naye kwa msaada,
Aliahidi kusaidia wakati baada ya kumueleza kila kitu, nilimpa kila alichouliza na akafanya kazi yake, sasa mume wangu ananipenda sana na ananitendea kwa Matunzo. Nyumba yangu ni ya amani na imejaa furaha, shukrani zote kwa Dk DAWN,

Wasiliana naye ikiwa una tatizo lolote kwa sasa. Yeye ni WhatsApp: +2349046229159
Barua pepe: dawnacuna314@gmail.com