Friday, August 23, 2013

MSHINDO WA AJALI


MSHINDO WA AJALI
Ndugu zangu wapendwa, salamu nazitoa kwenu ninyi nyote zikiniacha mimi ndugu yenu nikiwa katika hali ya kufikiria kwa nini tuko hapa? Salaam ziwafikieni nyote mlioko shambani mkitafuta riziki kwa kutumia jembe la mkono, mkilima katika shamba lenye miba mingi, mkitokwa jasho sehemu karibu zote za miili yenu, na kuliramba jasho litiririkalo kutoka vichwani mwenu, pia salaamu ziwafikie wafugaji ambao kutwa nzima mnazunguka na mifugo yenu porini huku mkitafuta marisho na maji ya kuwapa ng’ombe, mbuzi, kondoo na punda wenu uhai. Lakini haya yote mnayakosa kwa sababu hali ya mazingira yetu ya asili imebadirika na kuwa ya UTANDAWAZI,

Salaam nyingine za dhati nazituma kwa waalimu wote, madaktari, wafanyakazi bandarini, wajasiliamali, bila kuwa sahau wadogo zangu wanaoshinda katika masazo ya watu warukao kutwa nzima na midege yenye raha duniani, salaamu hizi ziwafikie akina mama wote mkiwa katika wadi ambazo hazina utofauti na jela, mwisho ningependa kuwapa salaamu za upendo ndugu zangu ambao kutwa wanawindwa mithili ya digidigi na viungo vyao kuwa vyanzo vya mapato ya wajinga wachache ambao wanalirudisha nyuma taifa changa lenye zaidi ya miaka arobaini.

Hapana wa mwisho ni hawa watoto ambao wazazi wao wametangulia mbele ya haki ama walitupwa jalalani na wazazi ambao walizitia nywele zao kemikali na kuziharibu akili zao na kuwa bora ya kichaa anayeandika namba za usajili za kila gari inayo katisha mbele yake. Watoto hawa waliokolewa kwa kuokotwa na kuokolewa kutoka katika midomo ya nguruwe, na mbwa koko ambao kutwa nzima wanacheza jalalani. Kwa pamoja nasema Salaamu.

Ndugu zangu labda nianze kwa kusema HERI KULIMIA NG’OMBE ULIYECHAGULIWA NA MTU KWA LENGO LA KWENDA KULIMA SHAMBA UKWENI NA NG’OMBE HUYO AKALALA SHAMBANI, KULIKO KULIMIA NG’OMBE ULIYEMCHAGUA MWENYEWE KUTOKA KATIKA ZIZI LENYE  NG’OMBE WENGI WENYE AFYA NJEMA AKALALA SHAMBANI TENA UKWENI.”
Hapana! Hapana! Hapana! Narudia tena hapana, hatutoruhusu tena kaka ukatutie aibu ukweni ni heri kulimia mbuzi hawa labda tutaweza kulimaliza shamba hata kama ni kwa muda mrefu tutamaliza kulima.

Ndugu zangu ajali iliyotokea mwanzo haikuwa na mshindo kama hii iliyotokea leo asubuhi, kwani mshindo wake umesikika mbali kwani hata jirani anashangaa, hebu nikuulize swali ni vipi dereva aliyesababisha ajali kubwa iliyouwa watoto zaidi ya sitini kati ya wale mia waliokuwa wakisafiri kwenda katika nchi ya ujuzi kwa lengo la kusaka taaluma ambayo ingewafanya wajitegemee baadaye na kuwa kizazi bora apewe tena usukani na kuliongoza gari hilo huku dereva huyu akiwa amefungwa majeraha na madakitari bingwa kutoka nje ya nchi ya watu weusi? Dereva aliyekatika mkono harafu anang’ang’ania gari?  Eti jamani swali hili jibu twalijua?

Kweli asiyeona akioneshwa haoni, kwa huzuni tuumalizeni msiba matanga tuyaanueni maana hatuwezi kujua nini akifanyacho kobe pindi awapo kimya ndani ya jumba lake huku miguu na kichwa chake vikiwa ndani labda tusuburi jibu. Maana tuliyemkabidhi silaha ndiye huyu  anayegeuka na kutujeruhi anayetuuzia kuni zetu, anayetuuzia maji yetu, anayetuuzia ardhi yetu, anayetuuzia urithi wetu ndiye huyu anayecheka nasi wakati wa kulia kwetu ni vipi kijana  kuoga na kuvaa nguo safi pindi uendapo kumposa binti wa jirani ilihali hali yako inafahamika, ni heri yule aliyesema akipata nauli mjini kwa mjomba atakwenda kuliko sisi tulioko huku tunywao maji yaliyochanganyika na kemikali kutoka katika migodi waliyopewa wageni, tulao mlenda na kulala, tulimao na bei tukapangiwa, tuingiao baharini na kuhatarisha maisha yetu kwa kucheza na mamba, tufikapo ufukweni mwatusubiri kwa bei chini, tuwakumbatiao watoto wachanga ambao wanalia kwa uchungu wakiwatafuta matiti ya  mama zao katika vifua vya wanaume maana sisi hatutaki kusafiri. Tulichoka katika safari tuliyosafiri jana dereva akiwa huyu! Huyu!, hebu watazame bibi zangu wale hawana hamu ya kusafiri tena kwenda kumuuona mjukuu wao aliyezaliwa, nashangaa hata babu zangu walio mkabidhi mkuki dereva huyu siku yake ya kwanza kukabidhiwa gari aliendeshe salaama na alifikishe salaama hawataki tena kupanda gari la dereva waliye mwamini.

Zaidi  ni hawa mama zangu wanaotoa machozi mabichi yaliyosababishwa na dhuruma na mwedo wa kasi aliokuwa nao dereva huyu katili ambaye mara nyingi mwendo kasi wake hushangiliwa na wapiga debe wachache ambao hutudagaya kuwa gari hili ni zuri halina tatizo, lina nafasi za kutosha maji na chakula tutavikuta humo, ikiwa wao hawasafiri na hubakia kituoni hapo, na kuanza kutoa sifa kama zilezile katika gari jingine. Mama zangu  walishuhudia watoto wa wanawake wenzao wakigongwa na kusagwasagwa kama mawe mgodini na huyu dereva msifika, mimi na hawa wote tumeamua kupiga hatua mbilimbele kuelekea magerezani ambako wapo ndugu zetu waliofungwa bila hatia, kuiamuru makama iwaachie huru ili waweze kufanya kazi za kimaendeleo kuliko kula chakula ambacho wake zao walioachwa wakiwa wajawazito wakilima  na kuipinda migongo yao iliyo wabeba watoto waliodhoofika kwa kukosa lishe  bora.

Kwa pamoja tunasema watoke! Watoke! Watoke! Watoke wawe huru kwani babu zetu waliokufa wakipigania ardhi yetu wameamua kutuunga mkono, wanasiasa waliouliwa kwa hila wameamua kuwa mbele yetu na maandamano makubwa yatafanywa na watoto wachanga siku yao ya watoto Duniani. Watoto wameayaona maovu yenu enyi tembo mnao angusha miti katika mbuga yenye amani, wameona wizi muufanyao katika rasilimali za nchi yao ambayo kila kukicha mwasimama majukwaani na kupayuka “WATOTO NI TAIFA LA KESHO” hivyo tulitunze na kulilinda, watoto wamechoka na elimu ya kishenzi inayotolewa, wanashangaa ni kwanini nyote mlioko madarakani mnajua kusoma, kuhesabu na kuandika lakini wao kila kukicha wanaandikwa magazetini tena magazeti yasiyo na uhuru wa habari ooh! ufahulu umeshuka, tuunde tume, tufanye tafiti, watoto wamefanya tafiti na kugundua kuwa tume hasifundishi, tafiti zimetosha maana karatasi na vifaa vinavyotumika kufanyia tafiti ni heri zitumike kuboresha mazingira ya ufundishaji na ujifunzaji.

Watoto wanayo michezo na burudani nyingi za asili ambazo walikuwa wakicheza wakati wa mbalamwezi, michezo iliyowafanya wakawa na miili kakamavu, hawakuwabana mama zao majikoni pindi waandaapo chakula. watoto walicheza kwa pamoja tena kwa umoja, walijifunza malezi hata kabla ya kuwa walezi, mama aliigiza umama na baba aliigiza ubaba watoto waliigiza utoto yote hayo yalifanyika katika familia iliyoundwa na mama mtoto, baba mtoto, na watoto. Ikumbukwe kuwa hakuna aliyewafundisha bali walirithi toka kizazi kimoja hadi kingine. Kutokana na mambo yote yaliyowakera watoto hawa wameamua kuandika barua na wanaomba isomwe na kila ajuaye kusoma wakiwemo kaka, dada, mama, baba, mjomba, shangazi, bibi, babu na ndugu jamaa na marafiki wote.

                                     BARUA YA WATOTO KWA WAZAZI

 Wapendwa baba na mama zetu, salaam.

Salaam zetu ziwafikie wazazi wetu baba na mama, mkiona vema mzifikishe kwa babu na bibi, kama babu na bibi zetu watazipokea basi wazifikishe kwa mizimu yetu iliyotuachia imani zetu, na mizimu yetu izifikishe salaamu hizi mahali aishipo Mungu wa miungu asante,

Dhumuni la barua hii ni kuwataarifu kuwa  kutokana na kishindo cha ajali  iliyotokea siku chache zilizopita na kuwaangamiza kaka zetu na dada zetu waliokuwa na nia njema ya kuusaka ujuzi wa kitaaluma lakini cha kushangaza tunaona tume zinaandaliwa na mapesa mengi yanatolewa kwa ajali ya kamati teule ya mtendaji mkuu wa kijijji chetu. Sisi watoto wenu tumeamua kwa pamoja na kwa moyo umoja kuingia barabarani kumshinikiza dereva aliyeshikilia usukani aachie ngazi ili gari letu liendeshwe na sisi wenyewe watoto mliodhani hatuyaoni yanayotendeka humu kijijini. Katika maandalizi ya siku yetu ya watoto duniani tumeamua tusile wali, soda, kuku, chips, nyama ya ng’ombe, nyama mbuzi, vileo, na mayai toka ughaibuni yanayoandikiwa pesa nyigi wakati sisi tu vibogoyo! wala hatutonyonya maziwa ya mama zetu yaliyojaa uchungu wa maisha  usababishwa na dereva katili tuliyemshuhudia tukiwa tu katika matumbo yenu.

Wazazi wetu katika sikukuu hiyo tutahitaji kuona vipaji kutoka miongoni mwetu kwani ngoma zetu zimeeharibiwa na utamaduni toka nje sasa mwacheza viduku, mwaimba kwa kufoka, mwalilia mapenzi badala ya kuhiza maendeleo mimi Kirundumusi ni shuhuda wa hayo myatendayo mchana kweupe na usiku pia, sisi watoto kwa macho yetu wenyewe macho yenye kujaa ukungu mkidhani hatuyaoni matendo juani, tuliyaona hayo na tumeamua kubadilika na katika risara tutakayo isoma mbele ya mgeni wetu rasmi si risala kama zenu mlizozoea kuimba rushwa, ufisadi, huduma za jamii, na kuwahurumia watoto na wamama wajawazito kwa kuandika jumbe fupi katika simu zenu za gharama na kuomba misaada ya vyadarua toka nchi za magharibi. Katika risala yetu tutazungumzia sera ya lugha ya kiswahili ambayo ndio muhimili wa maendeleo ya taifa letu watoto, sera itakayokuwa tofauti na yenu mnayoburuzwa kwa kukariri lugha msizozijua, pia tutahakikisha sisi watoto tunaurudisha mfumo wa elimu mlio upuuza na kuanza kuwaburuza kaka na dada zetu waliopata ajali pasipo wao kuhiari, sisi tutahakikisha mfumo wa KKK tatu unarudishwa kwa wajinga wasiojua unaitwa KUSOMA, KUANDIKA NA KUHESABU.
Wenu wanenu tuliotoroka katika matumbo yenu yaliyo jaa majipu ya maumivu, hasira, kisasi, huzuni, kwa pamoja tunasema tumeaua! tumeamua! kupambana hatutayaogopa mabomu ya machozi, kama ni risasi za moto sisi pia tu moto hivyo dawa ya moto ni moto na hivyo vitoa moshi twavijua vizuri kwani dalili ya moto ni moshi.

       Na, kapele harry, simu 0763891415
                                    Barua pepe, hkapele@gmail.com
                                    Blog, www.kapeleh.blogspot.com







No comments: